Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia Award Karonga, ambaye ni kiongozi mwandamizi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kwa tuhuma za uchochezi na makosa mengine ya kijinai.
Award Karonga, ambaye ni mkazi wa Katumba, anashikilia nyadhifa za Katibu wa CHADEMA Wilaya ya Rungwe na Makamu Mwenyekiti wa Hamasa Taifa wa chama hicho, kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa leo, Januari 30, 2026, na Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya

Kiongozi huyo ambaye baadhi ya viongozi wa CHADEMA kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii wamemtaja pia kama mlinzi wa Tundu Lissu, Mwenyekiti wa CHADEMA taifa aliyeko gerezani kwa tuhuma za uhaini, alikamatwa, Januari 29, 2026, majira ya saa nne asubuhi katika maeneo ya Mtaa wa Katumba, Kata ya Ibighi, Tukuyu wilayani Rungwe.
Jeshi la Polisi limebainisha kuwa kukamatwa kwa Karonga kumetokana na tuhuma mbalimbali za kijinai zinazomkabili, ikiwemo uchochezi. Taarifa hiyo haikufafanua kwa kina matukio mahususi ya uchochezi anayotuhumiwa kwayo, lakini imesisitiza kuwa makosa hayo ni ya asili ya kijinai.
“Upelelezi unakamilishwa ili hatua zaidi za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake”, imeeleza taarifa hiyo iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Benjamin Kuzaga.