Wizara ya uchukuzi imesema Bunge la Tanzania limeitaka serikali kuhakikisha inaulinda mradi wa reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) unaotekelezwa na Shirika la Reli Tanzania (TRC).
Kauli hiyo imetolewa Februari 14, 2026 na Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile, wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu, iliyotembelea mradi wa SGR kwa lengo la kupata ufahamu na uelewa wa majukumu ya Shirika pamoja na hatua mbalimbali zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi ya miundombinu ya Reli.

Aidha Naibu waziri huyo amesema kwa niaba ya Serikali na Waziri wa uchukuzi, amepokea hoja ya kamati inayoitaka serikali kuhakikisha inatoa huduma bora, kuzingatia ubora katika manunuzi ya vichwa ama mabehewa, na katika hatua nyingine, amepokea maelekezo ya kamati yanayoitaka TRC kushirikiana na taasisi nyingine ili iweze kusafirisha mzigo kwa Watanzania na nchi jirani.
Awali Kamati ya kudumu ya Bunge ya miundombinu iliyoongozwa na Makamu mwenyekiti wake Mhe. Abubakari Assenga, ilisema, inaunga mkono uwekezaji na mikakati TRCÂ iliyojiwekea kufikia mafanikio ikiwamo lengo la kufikia vichwa 30 vya treni ifikapo Machi 2026, kati ya mahitaji ya vichwa 58.

Aidha Kamati hiyo imeipongeza TRC Kwa kutoa ajira 894, kupandisha madaraha watumishi 3,153 kati yao 1,055 mserereko na 2,098 kawaida.
Mapema, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Tito Mateshi, akielezea mafanikio Shirika licha ya changamoto inazokabiliana nazo alisema kuanzia Desemba 2025, TRC meanza kujitegemea na kupunguza mzigo wa matumizi ya kawaida kwa serikali kwa wastani wa shilingi bilioni 12.9 kwa mwaka na kuwezesha fedha hizo za umma kuelekezwa kwenye miradi mingine ya maendeleo na kutoa motisha kwa Shirika kujiendesha kibiashara.
