Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima ameiagiza halmashauri ya Wilaya ya Mvomero kutangaza fursa za kiuchumi zilizomo katika halmashauri hiyo hususan kwa wafugaji, ili kuongeza tija katika shughuli za ufugaji, kukuza mapato ya halmashauri pamoja na kupunguza migogoro ya wakulima na wafugaji.
Malima ametoa agizo hilo Julai 10, 2026, wakati akifungua kikao maalum cha Baraza la Madiwani cha kupitia hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.

Amesema, ni muhimu kwa halmashauri kutumia vyema fursa zilizopo kwa kuwawezesha wafugaji kuinuka kiuchumi kupitia mipango yenye tija na manufaa ya moja kwa moja kwa jamii ya wafugaji.
Aidha, amesisitiza kuwa uwekezaji katika sekta ya mifugo na uanzishwaji wa mazingira rafiki kwa wafugaji utasaidia kupunguza migogoro kati ya wakulima na wafugaji, pamoja na kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya halmashauri na kubainisha kuwa hatua hiyo itachochea kiuchumi wa halmashauri hiyo na kuboresha hali ya wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mvomero Jaka Michael amesema Wilaya hiyo itaendelea kuimarisha ushirikiano kati ya viongozi na wananchi ili kuhakikisha fursa zilizopo katika sekta ya mifugo zinatumika ipasavyo.