Chama cha ACT Wazalendo kimemtaka Mkuu wa wilaya ya Kisarawe, mkoani Pwani Petro Magoti kuacha kile walichokiita ni oparesheni yake inayolenga kuuwa mila, desturi na kwa ujumla wake ni tamaduni za Tanzania
Taarifa ya chama hicho iliyotolewa mapema leo, Ijumaa Julai 19.2024 na Naibu Waziri Kivuli wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Monalisa Joseph Ndala imeeleza kuwa ACT Wazalendo inapinga vikali kauli za Mkuu wa wilaya huyo za kupiga marufuku utamaduni wa kabila la Wazaramo la kucheza Unyago
Amesema Unyago ni sehemu ya utamaduni wa Watanzania wengi hapa nchini ambao kwa kawaida unalenga kuwafunza vijana na watoto maadili, na kwamba maudhui yake hayahusishi kukatazwa watoto kupelekwa shule kama vile ilivyodaiwa na kiongozi huyo
Taarifa hiyo imeenda mbali zaidi kwa kueleza kuwa mamlaka ya uteuzi sambamba na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo kufuatilia kwa karibu mwenendo wa Mkuu wa wilaya ya Kisarawe Petro Magoti, na pale inapobidi hatua stahiki zichukuliwe dhidi yake.