Latest Posts

CHADEMA YAOMBA SIKU 21 KUJIBU HOJA ZA SAIDI NA WENZAKE MAHAKAMA KUU

Na; mwandishi wetu

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeomba siku 21 ili kujibu hoja zilizowasilishwa Mahakamani na waleta maombi Saidi Issa Mohammed na wenzake watatu (3) waliofungua kesi kwenye Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala ndogo ya Dar es Salaam wakiiomba Mahakama hiyo kutoa amri ya kusimamisha shughuli zote za kisiasa za chama hicho zinazoendelea hadi hapo shauri lao la msingi litakaposikilizwa na kutolewa maamuzi

Shauri hilo namba 8323 la mwaka 2025 linalowahusisha pia baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wadhamini wa CHADEMA kutoka Zanzibar iliitwa leo, Alhamisi Aprili 17.2025 chini ya Jaji Hamidu Mwanga, ambapo inaelezwa kuwa pande zote mbili zilihudhuria

Hata hivyo, Jambo TV imefanya jitihada za kuwasiliana na Mawakili wa pande zote mbili ili kujuwa kile kilichojili kwenye ‘kikao cha ndani’ baina yaa pande hizo mbili na Jaji, lakini Mawakili wa pande zote hawakutoa ushirikiano hitajika kwa wanahabari

Mawakili wa waleta maombi wakiongozwa na Gido Simfukwe na Shabaan Marijan inadaiwa kuwa walitumia ‘mlango wa nyuma’ kuingia Mahakamani hapo ili kukwepa waandishi, na hata walipotafutwa kwa simu kwa kutumiwa ujumbe mfupi wa maandishi (sms) au kupigiwa simu hawakupokea, na baadaye hawakupatikana hewani kabisa

Hata hivyo kwa upande wa utetezi (CHADEMA) waliwakilishwa na Mawakili wawili (2) mmoja kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu na mmoja kutoka kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu wa chama hicho

Mawakili hao ambao ‘waligoma’ kutaja majina yao wamesema wamepokea maelekezo kutoka kwa wakuu wao kwamba wawakilishe chama Mahakamani kisha wapeleke mrejesho, baada ya hapo chama kitatoa msimamo wake rasmi, hivyo wao kugoma kuongea na vyombo vya habari, hata hivyo Jambo TV imenukuu sehemu ya maelezo yao wakisema:

“Kesi ilikuja kwa ajili ya kutajwa, CHADEMA wanapokea nyaraka ambayo ni mashtaka au madai ya msingi kuhusiana na shauri husika baada ya hapo CHADEMA wameomba siku 21 kama kwa mujibu wa sheria ilivyo ili kujibu hayo madai au hayo mashtaka, kwahiyo  wameambiwa wawasilishe majibu yao kabla au kufikia tarehe 09/05/2025, na kesi itakuja tarehe 12/05/2025 saa 3 asubuhi kwa ajili ya kutajwa na kuangalia some oders kama zimezingatiwa”, ameeleza Wakili kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Sheria wa CHADEMA

Ikumbukwe kuwa, waleta maombi ambao ni Saidi Issa Mohammed (aliyewahi kuwa Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Zanzibar) na wenzake Ahmed Rashid Khamis na Maulida Anna Komu (Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini kutoka Zanzibar) wamefungua shauri hilo dhidi ya Bodi ya Wadhamini ya CHADEMA ambayo ni mdaiwa wa kwanza na mdaiwa wa pili na Katibu Mkuu wa CHADEMA

Waleta maombi wanaiomba Mahakama itamke kuwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimekiuka sheria inayohusiana na vyama vya siasa na Katiba ya chama hicho, kutokana na kile wanachodai kuwa uwepo wa mgawanyo usio sawa wa raslimali za chama na raslimali fedha kati ya Tanzania Bara na Zanzibar

Pia wanadai kuwa kuna ubaguzi wa kidini na kijinsia, pamoja na kutoa maoni na matamko yaliyo na nia ya kuvuruga Muungano kati ya pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Awali kabisa kabla ya kwenda Mahakamani, Jambo TV ilifanya mahojiano kwa njia ya simu na Wakili Gido Simfukwe anayewakilisha upande wa waleta maombi, ambapo akizungumza akiwa Zanzibar amenukuliwa akisema:

“Hili jambo ni kwamba kuna hawa Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya hicho chama (CHADEMA) wamekuwa wakitengwa hawa wanaotoka upande wa Zanzibar, kwa sababu bodi ile inaundwa na Wajumbe kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, sasa wao hawajaridhika na mgao wa raslimali za chama kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, kwa mfano mathalani kule Tanzania Bara kuna majengo, na wamenunua jengo jipya hivi karibuni lakini huku Zanzibar hakuna jengo lolote hata ofisi wamepanga, kuna magari ambayo yapo mengi tu wanatumia, kuna mashamba ambayo yapo maeneo mbalimbali ambayo ni mali za chama lakini kwa upande huu (Zanzibar) hakuna kitu chochote ambacho wanacho” -Wakili Simfukwe

“Hata ukiangalia katika mgao wa ile ruzuku, matumizi ya pesa yaani huku inaletwa Tsh. 4,000,00/- (Laki nne), pengine wanaweza wakaleta Tsh. 2,000,00/- (Laki mbili) kwa mwezi, hata mishahara ya wafanyakazi imekuwa ni shida, wengine wanadai mishahara yao hawajalipwa, sasa hii imewafanya hawa (wataja wake) wakasema hapana inatosha, tumepunjwa sana, kuna mapunjo ya mgawanyo wa raslimali za chama kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, kwahiyo hilo ndio limepelekea wakasema sisi twende Mahakamani tufungue kesi tudai mapunjo yote ambayo tumekuwa tukipunjwa na pia Mahakama itoe tamko juu ya mapunjo haya kwamba yanakwenda kinyume na sheria ya vyama vya siasa, yanakwenda kinyume na Katiba yenyewe ya CHADEMA, yanakwenda kinyume na miongozo ya Msajili wa Vyama vya Siasa pamoja na mustakabali mzima wa Muungano wetu kwa sababu, kwa sababu chama chochote kinachoanzishwa ni lazima kiwe chama cha kimuungano” -Wakili Simfukwe

Jambo TV inaendelea kufuatilia zaidi kile kinachoendelea kuhusiana na shauri hilo

Latest Posts

Don't Miss

Stay in touch

To be updated with all the latest news, offers and special announcements.

error: Content is protected !!