Na; Mwandishi wetu
Kesi ya uhaini Na. 19605/2025 inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa Tundu Lissu inaendelea tena leo, Alhamisi Februari 19.2026, kama ilivyo kawaida mbele ya jopo la Majaji watatu (3) wakiongozwa na Jaji Dastan Ndunguru
Kesi hiyo ambayo inasikilizwa kwa mfululizo, leo imekuja Mahakamani hapo kwaajili ya mashahidi wa Jamhuri kuendelea kutoa ushahidi wake, ambapo shahidi wa kwanza kwa siku hii, ambaye kimsingi ni shahidi wa 12 wa Jamhuri kwa ujumla wake ni Askari Polisi H. 937 Detective Koplo Vicent
Akiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu Ignas Mwinuka, shahidi huyo ambaye ni Askari Polisi ameieleza Mahakama kuwa yeye ana umri wa miaka 36, Dini yake ni Mkiristo, Mkazi wa Mbeya na anafanya kazi zake Police Central Mbeya
Anasema yeye, alijiunga na Jeshi la Polisi mwaka 2011, ambapo alipata mafunzo ya awali ya Upolisi katika Chuo cha Polisi Moshi (CCP Moshi) na kuhitimisha mafunzo hayo Machi 03.2012
Anasema baada ya kuhitimu rasmi mafunzo, akapangiwa Mkoa wa Mbeya, huku majukumu yake ya kila siku ikiwa ni kupeleleza kesi zinazofunguliwa pale kituoni, kukamata watuhumiwa na kutoa ushahidi Mahakamani
- 937 Detective Koplo Vicent ameieleza Mahakama kuwa mnamo Aprili 05.2025 akiwa anaendelea na majukumu yake ya kawaida kwenye Kituo cha Polisi cha Mwanjelwa, aliitwa na Mkuu wa Kituo na kupewa kazi ya kumtafuta ‘P9’
Anasema kulikuwa na taarifa fiche zilizoletwa kituoni hapo, zilizodai kuwa ‘P9’ anahamasisha kwenye vijiwe mbalimbali kuchochea Uchaguzi Mkuu wa 2025 usifanyike, ndipo akapewa maelekezo ya kumkamata
Anasema baada ya kupewa maelekezo hayo na Mkuu wa Kituo, Mkuu huyo wa Kituo pia alimpatia namba ya simu ya ‘P9’ ambapo Mkuu huyo wa Kituo alipata namba hizo za simu kutoka kwa msiri wake
Anasema kabla ya kumpigia na kumkamata, awali alimfuatilia na kugundua kuwa mtuhumiwa ni fundi Umeme, na ndipo yeye akatumia mbinu ya ‘kiupelelezi’ kumpigia mtuhumiwa huku akijitambulisha kuwa yeye ana tatizo linalohitaji fundi kama yeye kulitatua na wakakubaliana sehemu ya kukutana, na alivyofika alimueleza kuwa yeye si mteja kama alivyojitambulisha hapo awali, badala yake alijitambulisha kuwa yeye ni Askari Polisi (mpelelezi), akamuonesha kitambulisho chake cha kazi na kumueleza kuwa yuko chini ya ulinzi na kwamba anatuhumiwa kufanya uchochezi na kuhamasisha vurugu kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025
Shahidi huyo ameendelea kuieleza Mahakama kuwa, baada ya kumkamata mtuhumiwa (P9) hakutumia nguvu kwani alikuwa muelewa, akaongozananae na kumkabidhi kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi Mwanjelwa, na alipofika kituoni alimkabidhisha mtuhumiwa huyo kwa Mkuu wa Kituo aliyemtuma kazi awali, na yeye aliendelea na majukumu mengine, na huo ndio ukawa mwisho wa ushahidi wake Mahakamani,
Baada ya shahidi huyo wa 12 wa Jamhuri ambaye ni Askari Polisi H. 937 Detective Koplo Vicent kumaliza kutoa ushahidi wake akiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu Ignas Mwinuka, baadae Mahakama ilimpatia nafasi mshtakiwa Tundu Lissu ambaye anajitetea mwenyewe kwenye kesi hiyo kumuhoji shahidi maswali ya dodoso (Cross Examination)
Lissu: Nasikia we ni Home Boy wangu?
Shahidi: Ndio, ni sahihi kabisa, mimi ni Home Boy wako
Baada ya hapo Lissu alimuuliza shahidi kama atayafahamu maelezo aliyoandika kama akionyeshwa, ndipo shahidi alikubali na Lissu akawaomba Majaji shahidi aonyeshwe maelezo hayo,
Aliponeshwa maelezo shahdii alikubali kuwa ni maelezo yake na hivyo Lissu aliiomba Mahakama kupokea kielelezo na yalipokelewa na kipewa jina D11
Lissu: Waeleze Majaji kama kwenye maelezo yako kuna sehemu umeandika unafanya kazi Central
Shahidi: Hayapo
Lissu: Umesema tarehe 05/04/2025 ukiwa Kituo cha Polisi Mwanjelwa uliitwa na Mkuu wa Kituo ukiambiwa umtafute ‘P9’ kwa kosa la kuhamasha na kuchochea kuvuruga Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 usifanyike kwenye vijiwe mbalimbali, kweli si kweli?
Shahidi: Kweli
Lissu: Angalia kwenye maelezo yako
Shahidi: (anaangalia)
Lissu: Waeleze Majaji, nani aliyerekodi hayo maelezo yako?
Shahidi: Niliandika mimi mwenyewe
Lissu: Mtu anayeandika maelezo huwa anapewa onyo sio..
Shahidi: huwa hakuna onyo
Lissu: Hakuna maneno kama ‘nitasema kweli, kweli tupu nisiposema kweli nishtakiwe
Shahidi: Sio onyo
Lissu: huwa unasema nitasema kweli mbele ya nani?
Shahidi: mbele yangu mi mwenyewe..
Lissu: Nataka nijue huwa unasema mbele ya nani?
Shahidi: Kwa kuwa haya maelezo ni ya kwangu..sijakuelewa
Lissu: Hayo maneno unayatamka mbele ya nani?
Shahidi: Sio lazima utamke mbele ya mtu
Lissu: Unafahamu kitu kinaitwa PGO (Police General Order)?
Shahidi: Ndio naifahamu
Lissu: Kwenye PGO, ni kweli au si kweli kwamba PGO 236 inasema yeyote anayeandika maelezo ya ushahidi lazima aandikwe na askari anayefanya kazi hiyo?
Lissu akampa shahidi kitabu ch PGO,
Shahidi: Hii PGO mshtakiwa ni ya Kingereza sasa kwenye lugha ya Kingereza nisije nikakudanganya
Lissu: IGP alijua unafahamu Kingereza
Shahidi: Ya Kiswahili ipo
Lissu: Kwa hiyo huwezi ukajibu kwa sababu hujui Kingereza
Shahidi: Siwezi,
Lissu: Kwa mujibu wa PGO mtu ambae maelezo yanarekodiwa ya ushahidi hawezi akajiandikia maelezo mwenyewe
Shahidi: Sifahamu
Lissu: Kwenye ushahidi mwishoni umethibitisha ‘mimi kolo Vicent nathibitisha kuandika maelezo yangu kwa usahihi na uaminifu chini ya kifungu cha 10(3)(C) cha CPA RE.2022
Shahidi: Sahihi
Lissu: Waeleze Majaji kama kwenye hiyo sheria kuna hicho kifungu
Shahidi: Haya maelezo nilipokuwa nayaandika 2025 hiki kifungu kilikuwepo
Lissu: Kilikuwepo?
Shahidi: Ndio
Lissu: Waeleze Majaji kama kuna mtu yeyote aliyeshuhudia ukiandika hayo maelezo
Shahidi:…
Lissu: Wakari unamkamata alikuwa anafanya kosa gani?
Shahidi: Alikuwa na kosa la kuchochea na kuzuia uchaguzi mkuu
Lissu: Ulimkamata akiwa anachochea?
Shahidi: Njama, kwa muda huo alikuwa hachochei
Lissu: Swali langu wakati unamkamata alikua anafanya kosa lolote
Shahidi: Alikuwa hafanyi kosa lolote
Lissu: Waeleze Majaji kama kwenye maelezo yako umetaja jina la huyo Mkuu wa Kituo cha Polisi Mwanjelwa
Shahidi: Kwenye maelezo hakuna
Lissu: Na kwenye ushahidi wako umetaja jina?
Shahidi: Sijamtaja
Lissu: Umeeleza huyu mtuhumiwa P9 alikua anafanya/amefanyia kosa
Shahidi: Sikufafanua
Lissu: umesema alikua kwenye vijiwe
Shahidi:…
Lissu: Waheshimiwa Majaji namsomea shahidi maana ya kijiwe kwa mujibu wa Kamusi Kuu ya Kiswahili iliyotolewa na BAKITA (Mahali ambapo watu hasa vijana wasio na kazi hukaa pasi kufanya kazi), swali langu Mbeya ina vijiwe vingapi?
Shahidi: Sifahamu
Lissu: Waeleze Majaji kama umetaja alikua ameenda kwenye kijiwe gani?
Shahidi: Sijataja
Lissu: Waeleze Majaji kama umetaja tarehe ya huyu P9 aliyofanya hayo makosa
Shahidi: Nimetaja tarehe 05
Lissu: Tarehe 05 ndio siku uliyotumwa ukammakate, tusipotezeane muda
Shahidi: Tarehe 05 siku hiyo hiyo
Lissu: P9 alipanga njama na nani?, maana njama haipangwi na mtu mmoja
Shahidi: haijaelezwa
Lissu: Kuna kosa katika nchi hii la kuzuia Uchaguzi?
Shahidi: kosa lipo
Lissu: Sheria gani?
Shahidi: Sheria ndo siijuwi lakini kosa lipo
Lissu: Nikikuambia kuwa kwa sheria za Tanzania, kuzuia Uchaguzi si kosa popote pale utabisha?
Shahidi: Kosa lipo
Lissu: Waheshimiwa Majaji naomba nimuoneshe shahidi Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024 iliyosainiwa na ‘Mama’, na kwenye sheria hii hakuna sehemu yoyote iliyosema kuzuia Uchaguzi ni kosa
Shahidi: hilo sijuwi
Lissu: (anampatia shahidi Sheria ya kanuni ya adhabu aipitie na kueleza kosa la kuzuia Uchaguzi)
Shahidi: shahidi hii ni ya Kiingereza, kama kuna ya Kiswahili lete
Lissu: Ieleze Mahakaman kuwa P9 hakupelekwa Mahakamani kabisa?
Shahidi: Sijuwi, mimi jukumu langu lilikuwa kumfikisha kituoni
Lissu: unajuwa kwamba huyu P9 hakupelekwa Mahakamani popote badala yake amekuwa shahidi wa kesi hii?
Shahidi: sijuwi
Lissu: unajuwa kosa ambalo nimeshtanalo?
Shahidi: najuwa unashtakiwa kwa uhaini
Lissu: nimefanya matendo gani?
Shahidi: siyajuwi yote
Lissu: Umekuja kufanya nini?
Shahidi: kuna machache nafahamu
Lissu: Yapi
Shahidi: Nachofahamu ni kwanba unashtakiwa kwa kosa hilo kutojana na kauli zako
Lissu: Mimi natoa kauli kwa maelfu, unazungumzia kauli yani?
Shahidi: Video mojawapo ukihamasisha utakinukisha uchaguzi wa mwaka hu sijui utakuaje vitu kam hivyo
Lissu: Umeleta hiyo video Mahakamani?
Shahidi: Niliiona tu, sijaiwasilisha
Lissu: Waheshimiwa Majaji, sina maswali mengine
Baada ya mshtakiwa Tundu Lissu ambaye anajitetea mwenyewe kwenye kesi hiyo kumaliza kuhoji maswali ya dodoso, Wakili wa Serikali Mkuu Ignas Mwinuka alimgeukia shahidi na kumuuliza ‘umeulizwa kuhusu takwa la onyo hebu ieleze Mahakama takwa la onyo huwa linatumika katika maelezo gani?
Shahidi katika majibu yake aliieleza Mahakama kuwa huwa linatumika katika maelezo ya mtuhumiwa, na yeye ameandika maelezo ya shahidi.
Kesi hiyo inaendelea ambapo shahidi wa pili kwa siku ya leo, ambapo kwa ujumla wake ni shahidi wa 13 wa Jamhuri anaendelea kutoa ushahidi, huyu ni shahidi wa siri, dereva Bodaboda kutoka Mbeya.