Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma limetangaza kuanza uchunguzi wa kina kufuatia taarifa za kutoweka kwa mfanyabiashara wa Soko la Buzebazeba, Mahamoud Juma Abdallah (25), anayedaiwa kuchukuliwa na watu wasiofahamika akiwa eneo lake la kazi.
Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, ACP Philemon Makungu, Februari 20, 2026, tukio hilo liliripotiwa rasmi Februari 19 majira ya saa 09:00 asubuhi. Mahamoud, ambaye ni mkazi wa Mtaa wa Mwasenga katika Manispaa ya Kigoma Ujiji, anadaiwa kutoweka katika mazingira tatanishi akiwa kazini kwake sokoni.
“Uchunguzi utakapokamilika utabaini ukweli wa tuhuma hizo. Aidha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma linatoa wito kwa yeyote mwenye taarifa au ushahidi ambao utasaidia uchunguzi kukamilika kwa wakati aufikishe Polisi ili uweze kufanyiwa kazi kwa haraka”, imeeleza taarifa hiyo.
Wakati msako na uchunguzi ukiendelea, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma amewataka wakazi wa Kigoma Ujiji na mkoa mzima kwa ujumla kuwa watulivu. Polisi wameahidi kutoa mrejesho mara baada ya ukweli wa tukio hilo kubainika na hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wahusika wowote watakaobainika kuhusika na suala hilo.