Bodi ya Maji bonde la Rufiji imewataka wakazi wa mkoa wa Njombe kufuata sheria ili kuepuka adhabu wanazoweza kuzipata mara baada ya kubainika uvunjifu wa sheria ikiwemo kulima karibu na vyanzo vya maji.
Wito huo umetolewa na Edward Wasele,afisa sheria kutoka bodi hiyo wakati wakiendelea na zoezi la upandaji wa miti rafiki wa maji kwenye chanzo cha maji Ijunilo kilichopo ramadhani mjini Njombe unaofanywa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mjini Njombe (NJUWASA)

“Maeneo mengi inatokea tumeweka alama,mabango lakini bado watu wanaendelea kukiuka,kwa hiyo tunawaomba wananchi tunaamini ni wahifadhi waunge mkono hizi juhudi ambazo zinafanywa na serikali”
Kwa upande wake,Mkurugenzi wa NJUWASA Mhandisi Robert Lupoja, amesema zoezi hilo la upandaji miti ni muhimu ambapo wanatarajia kupanda miti 80,000 kwenye vyanzo vyote nane vya mji huo ili kuvirudishia vyanzo uwezo wa kuzalisha maji.
Nao baadhi ya wakazi wa Njombe walioshiriki zoezi la upandaji miti akiwemo Elizabeth Kilindi pamoja Solanus Mhagama wanasema zoezi hilo ni muhimu sana katika kulinda na kutunza vyazo vya maji kwa kuwa madhara makubwa ikiwemo upungufu wa maji umeonekana.
