Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara imeombwa kutoa ushirikiano na ufafanuzi kwa wawekezaji wa vivutio vya utalii, hasa kwenye maeneo ya fukwe, ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza, hasa za usalama.
Wito huu umetolewa wakati wa tamasha la Nyangumi mwaka 2024 lililofanyika kwenye viwanja vya Mashujaa, Manispaa ya Mtwara Mikindani.
Mwakilishi wa Meneja Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu Tanzania, Deodat Mmanda, amesema kwamba vipo visiwa viwili ambavyo bado havijapata wawekezaji kutokana na changamoto mbalimbali, hasa za kiusalama. Mmanda alitoa rai kwa wananchi wa mkoa huo kufuata utaratibu wa uvuvaji na kuepuka makazi kwenye maeneo ya visiwa, akisema,
“Gharama kubwa inatumika katika kulinda hifadhi hizi kwa ajili ya kunufaika kiuchumi kwa kizazi cha sasa na kijacho.”
Aidha, Mmanda alisisitiza kuwa Marine Park wako tayari kuimarisha miundombinu na kutatua changamoto zilizopo, akisema kuwa kufanya hivyo kutafanya maeneo haya kuwa bora zaidi na kuvutia wageni.
Dkt. Edward Kohi, Mkurugenzi wa Kitengo cha Utafiti na Mafunzo Wizara ya Maliasili na Utalii, ambaye pia alikuwa mgeni rasmi, alieleza kwamba wizara yake iko kwenye mpango wa kutembelea mikoa ya Mtwara na Lindi.
Mpango huu unalenga kuhakikisha vivutio vyote vilivyopo vinatangazwa na kuendelezwa. Dkt. Kohi aliwaomba viongozi wa mkoa kutoa ushirikiano wa karibu ili kuandaa mpango wa kuendeleza vivutio vilivyopo.
“Kuonyesha kuwa na rasilimali ni hatua moja, lakini kuvifanya kuwa kivutio cha watu ni hatua nyingine,” alisema Dkt. Kohi.
Aliongeza kuwa wataalamu watakuja kuhakikisha rasilimali zilizopo zinabadilishwa kuwa vivutio vya kuvutia na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Mtwara na Lindi.
Tamasha hili, lililokusanya wadau wa utalii na wananchi, limekuwa jukwaa la kutoa mwito wa ushirikiano na kuimarisha sekta ya utalii katika mkoa huo, huku kukiwa na matumaini ya kuongeza manufaa ya kiuchumi kwa eneo hilo.