Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Stephen Wasira, ameeleza kuwa mchakato wa maridhiano ya kitaifa haupaswi kutumika kama kinga ya kukwepa uwajibikaji wa kisheria kwa wale waliohusika katika uhalifu.
Katika mahojiano maalumu na gazeti Mwananchi, Wasira amepinga vikali dhana ya kuwepo kwa “kesi za kisiasa” nchini. Kauli yake inaelezwa kuwa jibu kwa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bara, John Heche, ambaye hivi karibuni aliweka sharti kuwa maridhiano hayawezi kufanyika hadi Mwenyekiti wao, Tundu Lissu, aachiwe huru.
“Hakuna kesi za siasa, ukifanya makosa ukavunja sheria inakuwa kesi ya siasa? Kesi ya siasa huwa haiendi mahakamani, nenda nchi zote. Kesi ya kisiasa haikupi haki ya kujitetea,” amesema Wasira.
Wasira amefafanua kuwa maridhiano yanapaswa kuongozwa na Serikali kwa sababu jamii nzima iliathirika na vurugu za Oktoba 29 na 30 mwaka jana, na si wanasiasa pekee.
“Maridhiano sio mbadala wa sheria, maridhiano hayabadili sheria, hakuna aliye juu ya sheria, ukiwa kiongozi wa kisiasa unapaswa kuheshimu sheria, ukikosea utashtakiwa na kukamatwa kama raia mwingine,” amesisitiza Wasira akiongeza kuwa Tanzania ina watu zaidi ya milioni 60 na sio kwamba wanaokosea ni wanachama wa chama fulani pekee, akisisitiza wapo wanachama wa CCM waliopo magerezani.