Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Vijana Ajira na wenye Ulemavu Patrobas Katambi amefunga mafunzo ya lugha ya alama kwa watumishi wa Suma JKT Guard ltd jijini Dar es Salaam ambapo wahitimu 32 wamehitimu mafunzo ya miezi miwili na kutakiwa kwenda kuyatendea haki mafunzo hayo kwa watu wenye ulemavu.
Ameyaeleza hayo alipokuwa akifunga mafunzo hayo ambapo alisema hatua zilizochukuliwa ni pamoja na Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023 kuanzishwa kwa muongozo wa lugha za alama ambao upo hatua za ukamilishwaji.
Katambi amesema kukosekana wataalamu wa lugha za alama sehemu za kutolea huduma inasababisha baadhi ya makundi maalumu kukosa huduma stahiki.
Katambi amesema Ili kundi hilo lipate huduma sawa na wengine mikakati ya kitaifa ya mafunzo ya lugha za alama kwa watumishi wa umma na watoa huduma tayari hatua zimeanza kuchukuliwa.
Naibu Waziri huyo aliipongeza Taasisi ya Foundation for Disabilities Hope (FDH) kwa kutoa mafunzo hayo kwa watumishi hao ambao wanatoa huduma katika taasisi mbalimbali za kutolea huduma kwa watu tofauti akiwamo makundi maalumu.
Pia Katambi amesisitiza waajiri sekta mbalimbali za umma na binafsi nchini kuendelea kuwapatia watumishi wake mafunzo ya lugha za alama ili wananchi wa makundi maalumu wapate mawasiliano kikamilifu wanapohitaji huduma.
Mwakilishi wa Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ambaye pia ni Mkurugenzi wa Shirika la uzalishaji mali wa Jeshi hilo Kanali Robert Kessy amesema mafunzo hayo yanakwenda kuwa na mabadiliko kwa watumishi waliohitimu ambao watawasaidia makundi maalumu sehemu za kutolea huduma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya FDH MaIko Hosea alisema kabla ya kuanza kutoa mafunzo ya alama kwenye maeneo mbalimbali, taasisi hiyo ilifanya utafiti na kubaini watu wenye ulemavu hawapati huduma kikamilifu kutokana na vikwazo mbalimbali.
Hosea alibainisha baadhi ya vikwazo walivyobaini kuwa ni pamoja na watoa huduma kutokuwa na uelewa wa lugha za alama na hivyo wenye ulemavu wa kusikia kutopata huduma stahiki.
Utafiti huo pia ulibaini uelewa mdogo kuhusiana na Sheria namba 9 ya mwaka 2010 na miongozo ya watu wenye Ulemavu inayotaka uboreshaji wa Huduma za mawasiliano baina ya wenye Ulemavu na watoa huduma Hali inayosababisha makundi maalumu kupata huduma hafifu.
Pamoja na mapambano ya kutoa mafunzo taasisi hiyo imeeleza kuwa inakabiliwa na kikwazo cha ushirikiano mdogo kutoka kwa baadhi ya mashirika na Taasisi za Umma kwani wengi wao hawaoni umuhimu wa mafunzo hayo kwa watumishi wao.