Latest Posts

WAZIRI GWAJIMA: VIJENGWE VYUMBA VYA KUNYONYESHEA VYA AKINA MAMA MAGEREZANI

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema kwamba wanawake na wanaume wanategemeana katika kazi ili kuleta maendeleo endelevu.

Waziri Dkt. Gwajima ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza nchini, uliofanyika Septemba 2, 2024 jijini Dodoma.

Waziri Dkt. Gwajima amebainisha kwamba hali ya kutegemeana inatokana na tofauti ya utekelezaji wa majukumu katika maeneo mbalimbali kati ya mwanamke na mwanaume, ambapo husababisha wanawake kupewa msukumo wa kipekee katika kuhakikisha majukumu ya familia hayaathiri ushiriki wao katika nafasi za maamuzi na ujenzi wa taifa.

“Jambo hili linajulikana na Serikali, hali iliyochochea kutungwa kwa Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya Mwaka 2023, inayotoa dira ya usawa katika nyanja zote za maendeleo, ikiwemo elimu, afya, nafasi za maamuzi, na uchumi,” amesema Waziri Dkt. Gwajima.

Amesema sera hiyo imeweka mazingira wezeshi kwa wanawake na wanaume katika kutekeleza majukumu yao kulingana na mahitaji ya kijinsia.

Aidha, Waziri Dkt. Gwajima amemuomba Kamishna Jenerali wa Magereza kuangalia namna ya kujenga vyumba vya kunyonyeshea watoto mahali pa kazi katika miundombinu mipya ya Magereza. Hii ni sehemu ya mpango wa Serikali kusaidia afya za watoto na akina mama kupata utulivu ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Waziri Dkt. Gwajima amefurahishwa na uanzishwaji wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza, akisema kuwa ni matokeo chanya ya kazi anazozifanya na Wizara anayoiongoza, hasa jinsi sera na miongozo inayotolewa katika kufikia usawa wa kijinsia inavyotekelezwa kwa vitendo.

Kwa upande wake, Kamishna wa Huduma za Urekebu na Mwenyekiti wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza Taifa, Bertha Minde, amesema kwamba baadhi ya malengo ya mtandao huo ni kuongeza ufanisi wa kazi, kutambua mchango wa wanawake jeshini, kuleta usawa wa kijinsia katika utekelezaji wa majukumu, na kusaidia jamii katika kupunguza uhalifu.

Naye Makamu Mwenyekiti wa mtandao huo, Sp. Tekla Ngilangwa, akisoma risala ya mtandao, amebainisha kwamba Mtandao wa Wanawake wa Jeshi la Magereza ulioanzishwa mwaka 2018 ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha Kamati Ndogo ya Wakuu wa Magereza wa nchi za SADC kilichofanyika Lusaka, Zambia mwaka 2011.

Utekelezaji wa azimio hilo nchini ulijumuisha kuendeleza mikakati iliyopo kwenye Sera ya Maendeleo ya Wanawake iliyoanza kutumika mwaka 1992 na Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000.

Latest Posts

Don't Miss

Stay in touch

To be updated with all the latest news, offers and special announcements.

error: Content is protected !!