Serikali ya Burkina Faso imetangaza mpango wa kuchukua udhibiti wa migodi ya dhahabu inayomilikiwa na kampuni za kigeni, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha taifa linanufaika moja kwa moja na rasilimali zake, hasa sekta ya madini ambayo ni uti wa mgongo wa uchumi wa taifa hilo.
Akihutubia taifa kupitia televisheni ya kitaifa, Waziri Mkuu Jean Emmanuel Ouédraogo amesema serikali itaendelea kupanua majukumu ya Société de Participation Minière du Burkina (SOPAMIB), shirika jipya la madini la serikali, ambalo tayari limeshachukua usimamizi wa migodi mikubwa ya Boungou na Wahgnion, iliyokuwa chini ya kampuni ya Endeavour Mining ya Uingereza.
“Urejeshaji wa migodi ya viwandani kupitia SOPAMIB utaendelea,” amesema Ouédraogo. “Ni sehemu ya mageuzi ya kurejesha mamlaka ya taifa juu ya rasilimali zetu za asili.”
Mwaka 2023, Burkina Faso ilipitisha marekebisho ya sheria ya madini yaliyolenga kuimarisha udhibiti wa serikali, kuongeza ushiriki wa wataalamu wa ndani, na kuhamasisha uzalishaji unaoendeshwa na raia wa taifa hilo.
Licha ya kuwa hatua hizo zimeibua wasiwasi kwa wawekezaji wa kimataifa, serikali imesisitiza kuwa ni sehemu ya mkakati wa kupata faida halisi kutoka kwa sekta ya dhahabu, sekta ambayo imeendelea kustawi licha ya changamoto za kiusalama zinazoletwa na makundi ya waasi wa Kiislamu.
Tangu mapinduzi ya kijeshi ya mwaka 2022, Burkina Faso imebadilisha mwelekeo wa kidiplomasia kwa kujitenga na ushirikiano wa jadi na mataifa ya Magharibi na kuimarisha uhusiano wa kiuchumi na kiusalama na Urusi.
Wiki iliyopita, serikali ilitoa leseni ya uchimbaji kwa kampuni ya Nordgold kutoka Urusi, kwa mradi mkubwa katika eneo la Plateau-Central.
Katika hotuba hiyo, Waziri Mkuu alifichua kuwa Kampuni ya Kitaifa ya Vito vya Thamani ilikusanya zaidi ya tani 11 za dhahabu ndani ya robo ya kwanza ya mwaka 2024, kiasi kikubwa kikiwa kimetokana na wachimbaji wadogo.
Serikali pia ipo katika hatua za kuanzisha hifadhi ya dhahabu ya kitaifa, ikiwa ni mkakati wa kulinda akiba ya taifa na kudhibiti bei ya dhahabu katika soko la ndani.
“Ni lazima tuhakikishe kuwa wananchi wananufaika zaidi na sekta ya madini, badala ya kubeba tu gharama zake,” amesisitiza Ouédraogo.