
📌Kimetekelezwa na REA kwa gharama ya Tsh. Bilioni 25
📌DC Kilombero aipongeza REA, atoa wito kwa wawekezaji
📌Kimeimarisha upatikanaji wa umeme Ukanda wa Morogoro Kusini
Ifakara, Kilombero
Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imetumia shilingi bilioni 25 kujenga Kituo cha Kupoza Umeme 1x20MVA, 220/33kv pamoja na njia za kusambaza Umeme katika Wilaya ya Kilombero, hatua ambayo imeboresha upatikanaji wa umeme na kuondoa changamoto ya kukatika kwa nishati hiyo katika wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi.
Hayo yameelezwa leo Jumanne Machi 31, 2026 wakati wa ziara ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) waliotembelea mradi huo kujionea utekelezaji wake na tija yake kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika ukanda wa Morogoro Kusini.
“Fursa za uwekezaji wilayani hapa zimeongezeka baada ya kukamilika kwa kituo hiki, ninatoa wito kwa wawekezaji kujitokeza kwa wingi kwani tunao umeme wa uhakika na toshelevu,” amebainisha Wakili Kyoba.
Amesema kuimarika kwa huduma ya umeme kumechochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, hususan katika sekta za viwanda, uchimbaji madini, kilimo na huduma za kijamii.
Kwa upande wake, Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme kutoka REA, Mhandisi Deogratius Nagu, amesema gharama za mradi huo zinahusisha pia usimikaji wa mashine umba (transfoma) pamoja na mifumo yake ya uendeshaji, udhibiti na ulinzi, ujenzi wa njia za kusafirisha umeme za msongo wa kilovolti 33 zenye urefu wa kilometa 70 pamoja na gharama za mshauri elekezi.
Mhandisi Nagu amebainisha kuwa, kituo hicho ni cha kisasa, kikiwa na teknolojia kutoka nchi mbalimbali ikiwemo transfoma kutoka Bulgaria, mifumo ya udhibiti na ulinzi kutoka Hispania pamoja na mifumo ya switching (switchgears) kutoka Ujerumani.
“Kituo hiki kimeondoa changamoto ya upatikanaji wa umeme katika wilaya za Kilombero na Ulanga na kuwezesha wananchi kuendeleza shughuli za uzalishaji na kuongeza thamani ya mazao,” alisema Nagu.
Naye Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile, amesema uwekezaji huo unaonesha matumizi sahihi ya rasilimali za umma na mchango wa REA katika kusambaza huduma ya umeme vijijini.
“Tumeshuhudia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali kupitia REA, ni fursa ya maendeleo kwa wananchi ni muhimu tukachangamkia Uwepo wa umeme wa uhakika kujiletea maeendeleo,” amesema Balile.
Balile amesema REA imeonyesha mfano wa kipekee kwenye utekelezaji wa majukumu yake na kwamba kazi iliyokwishakamilika ni kubwa na manufaa yake yanaonekana na ametoa wito kwa Taasisi zingine za Serikali kuiga mfano huo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wanufaika wa mradi huo wameeleza namna ambavyo Mradi huo umekuwa mkombozi kwao.
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Kilimo Ifakara, Setina Ngailo, amesema huduma ya umeme imeimarika na kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme iliyokuwa ikiathiri shughuli za shule.
Kwa upande wake, Msimamizi wa Hospitali ya Kansa ya Good Samaritan, Father Charles Masawe, amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika umeongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya kwa kupunguza utegemezi wa jenereta.
Naye Meneja wa Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Bezelengule, Enos Machumu, amesema uzalishaji umeongezeka kwa kiasi kikubwa kufuatia kuboreshwa kwa huduma ya umeme, hali iliyorejesha wateja na kulinda mitambo dhidi ya uharibifu.
Kwa ujumla, mradi huo unatajwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika ukanda wa Morogoro Kusini, huku serikali ikiendelea na juhudi za kusambaza umeme katika vitongoji vilivyobaki ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi wote.