Kibaha, Pwani: Mei 7, 2025:
Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), imetambulisha kampeni yake ya ‘Wekeza NBC Shambani Ushinde’ kwa wakulima wa zao la ufuta mkoa wa Pwani ikiwa ni muendelezo wa jitihada za benki hiyo kuchochea kasi ya ukuaji wa sekta ya kilimo kupitia uchumi jumuishi unaochagizwa na huduma rasmi za kifedha.
Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo ilifanyika leo wilayani Kibaha ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Bw Nickson Simon ‘Nikki wa Pili’ huku pia ikihushisha uwepo wa wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo kutoka mkoa huo akiwemo Mrajisi Msaidizi wa Mkoa huo Bw Abdillahi Mutabazi, viongozi wa vyama vya msingi na vyama vikuu vya ushirika vya wakulima na wafugaji (AMCOS), pamoja na wadau wengine wanaoshiriki kwenye mnyororo wa thamani wa sekta hiyo muhimu.
Mkuu wa kitengo cha wateja wadogo wadogo na wakulima kutoka Benki ya NBC, Bw Raymond Urassa aliwaongoza maofisa wengine wa benki hiyo kwenye uzinduzi wa kampeni hiyo inayotoa fursa kwa wakulima wa zao la ufuta mkoa wa Pwani kushinda zawadi mbalimbali ikiwemo pikipiki na kompyuta mpakato ‘Laptops’
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Bw Nickson pamoja na kuipongeza benki hiyo kwa jitihada zake endelevu zinazolenga kuwasaidia wakulima na wafugaji katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo mkoa wa Pwani, alitumia muda mwingi kuwasisitiza wakulima mkoani humo kutumia vema mwamko wa taasisi za fedha katika kutoa huduma mbalimbali kwa wakulima ikiwemo kujiwekea akiba na kujipatia mikopo mbalimbali kwa nia ya kuendeleza kilimo chao.
“Kesho ya kila mtu inaandaliwa leo. Ni vema wakulima kama walivyo wafanyakazi wengine mtumie vizuri ukaribu huu unaoonekana sasa kati yenu na taasisi za fedha ikiwemo NBC katika kujiwekea akiba, kupata mikopo itakayowasaidia kukuza kilimo chenu na zaidi mnufaike na huduma nyingine za kibenki ikiwemo bima ya afya na bima ya mazao yenu. Naamini ujio wa kampeni hii utasaidia kuchochea ukuaji wa uchumi wa wadau mbalimbali wa sekta hii muhimu,’’ alisema.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mrajisi Msaidizi Mkoa wa Pwani, Bw Abdillahi Mutabazi alionyesha kuvutiwa zaidi na utoaji wa elimu kuhusu nidhamu ya fedha miongoni mwa wakulima mmoja mmoja na vyama vya ushirika hatua ambayo itawajengea uwezo wa kuona umuhimu wa kujiwekea akiba, umuhimu wa kutumia bima mbalimbali ikiwemo bima ya afya, bima za kilimo pamoja na kuwekeza kwenye zana za kisasa za kilimo.
“Hatua hii itasaidia kwa kiasi kikubwa kuhamasisha wakulima wetu kugeukia huduma rasmi za kifedha na hivyo kuchochea uchumi jumuishi. Hii ni hatua kubwa sana ikilinganishwa na tulipotoka miaka kadhaa iliyopita ambapo wakulima na wafugaji walikuwa hawaaminiki na taasisi za kifedha kutokana na kutokuwa waaminifu na wengine kutokuwa na dhamana.’’ Aliongeza.
Akifafanua zaidi kuhusu kampeni hiyo , Bw Urassa alisema walengwa wa kampeni hiyo ni wakulima wa zao la ufuta kupitia vyama vya msingi, vyama vikuu vya ushirika na mkulima mmoja mmoja ambao wanahudumiwa na benki hiyo.
“Lengo la kampeni hii ni kuwahamasisha wakulima wa zao la ufuta kwenye mkoa wa Pwani kutunza fedha zao kwenye mifumo rasmi ya kifedha hasa benki badala ya kutunza kwenye mifumo isiyo rasmi. Tunawakaribisha sana kufungua akaunti zao za NBC Shambani ili wawe kwenye nafasi ya kushinda zawadi hizi zikiwemo pikipiki na ‘laptop’’ Alisema.
Akizungumza kwa niaba ya wakulima hao, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Pwani (CORECU), Mussa Hemedi Mng’eresa aliwahimiza wakulima mkoani humo kutumia vema ujio wa kampeni hiyo kujinufaisha kupitia fursa mbalimbali zinazoambatana na kampeni hiyo ikiwemo zawadi, elimu ya fedha, mikopo na huduma nyingine ikiwemo bima za afya na mazao.