Latest Posts

SERIKALI YAITAKA BENKI YA EQUITY KUUNDA TIMU MAALUM YA KUSIMAMIA UWEKEZAJI SEKTA YA NGOZI

Serikali imeitaka Benki ya Equity na Bodi yake kuunda timu ndogo itakayojumuisha wawakilishi kutoka serikalini na benki hiyo, kwa lengo la kusimamia mchakato wa uwekezaji katika sekta ya ngozi, hatua inayolenga kuinua hali ya kiuchumi ya wafugaji nchini.

Hayo yamesemwa Julai 23,2025 jijini Dodoma na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt.Edwin Mhede, katika kongamano la ngazi ya juu kuhusu kufungua fursa za minyororo ya thamani ya mifugo na ngozi nchini Tanzania lililoandaliwa na Benki ya Equity.

Dkt. Mhede amesema kuwa timu hiyo itasaidia kuhakikisha wawekezaji na wazalishaji wakubwa wa ngozi nchini wananufaika na biashara hiyo huku wakiliinua taifa kiuchumi. Ameongeza kuwa mafanikio ya sekta hiyo yatategemea ushirikiano wa karibu baina ya wadau na kuepuka ubinafsi.

“Nawapongeza sana Equity Benki kwa kuonesha nia ya kuwekeza kwenye sekta ya ngozi. Naomba mshirikiane na wadau wengine ili mfanikishe kile mlichokusudia,” amesema Dkt. Mhede.

Aidha, ameeleza kuwa hadi kufikia jana, serikali imefanikiwa kuchanja mifugo milioni 16 katika maeneo mbalimbali nchini na zoezi hilo linatarajiwa kukamilika Oktoba mwaka huu.

Hata hivyo amesisitiza umuhimu wa wafugaji kuchanja mifugo yao ili kupata ngozi bora kwa ajili ya biashara ndani na nje ya nchi.

Dkt. Mhede ameipongeza Benki ya Equity kwa kuandaa kongamano hilo muhimu, na kuonesha utayari wa kushirikiana na serikali katika kuwezesha mitaji, kuboresha biashara za wafugaji, pamoja na kuimarisha minyororo ya thamani katika sekta ya mifugo.

“Kongamano hili ni fursa ya kipekee ya kufanya tathmini ya kina kuhusu hali ya sekta ya mifugo. Kupitia jukwaa hili, tunaweza kuona fursa zilizopo na changamoto zinazoikabili sekta, ili kwa pamoja tuweze kuchukua hatua sahihi za maendeleo,” ameeleza

Pia amesisitiza kuwa sekta ya mifugo ni uti wa mgongo kwa mamilioni ya Watanzania, hivyo ushirikiano wa karibu na taasisi kama Benki ya Equity ni msingi imara wa mageuzi chanya katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo Dkt. Mhede ametoa wito kwa wadau wengine kutoka sekta mbalimbali kuiga mfano wa Benki ya Equity kwa kuwekeza katika sekta ya mifugo, kwa kuwa ina fursa nyingi ambazo hazijatumika kikamilifu, hasa kwenye maeneo ya uzalishaji wa ngozi, usindikaji wa mazao ya mifugo, na upatikanaji wa masoko ya uhakika.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya Equity, Dkt.Florens Turuka, amesema kuwa benki hiyo imeona fursa nyingi katika sekta ya ngozi, hali iliyowasukuma kuwekeza moja kwa moja katika sekta hiyo ili kusaidia wafugaji kufikia maendeleo.

“Fursa zilizopo kwenye sekta ndogo ya ngozi ni nyingi sana, hivyo wafugaji wanapaswa kujitokeza kushirikiana nasi ili waendelee kukuza biashara yao,” amesema Dkt. Turuka.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Equity, Isabela Maganga amesema kuwa benki hiyo imejipanga kushirikiana na serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya mifugo, hasa zao la ngozi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupanua wigo wa biashara na kusaidia wananchi.

“Kama benki, tumejipanga kuhakikisha sekta ya ngozi inakua. Tumeamua kuwekeza kwa sababu tunatambua fursa lukuki zilizopo na tunataka kugusa maisha ya wananchi,” amesema Maganga.

Aidha amewataka wafugaji kuchangamkia fursa hiyo inayotolewa na benki hiyo ili waweze kupiga hatua katika biashara ya ngozi wanayofanya kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Latest Posts

Don't Miss

Stay in touch

To be updated with all the latest news, offers and special announcements.

error: Content is protected !!