Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Iringa imeendelea na zoezi la kuwatembelea na kuwashukuru walipakodi mbalimbali mkoani humo kwa kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa wakati
Shukrani hizo zimetolewa tarehe 17 Desemba 2024 baada ya Meneja wa TRA Iringa Bw. Peter Jackson akiwa ameambatana na meneja msaidizi Bw. Gwamaka Pholld kumtembelea mlipakodi Asas Group of Companies.
“Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na wafanyabiashara hasa kwenye ukusanyaji wa mapato, na ninaomba nifikishe kwako salamu za Kamishna Mkuu ambaye amesema yupo bega kwa bega na walipakodi wote na anawatakia heri ya sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya”, amesema Jackson.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Asas Group of Companies Bw. Salim Abri ameishukuru TRA kwa ushirikiano inaotoa kwa wadau wake huku akiishauri serikali kupitia TRA iweke jitihada za makusudi kabisa kuhakikisha inakusanya kodi ya ushuru wa bidhaa kutoka kwa waagizaji/waingizaji wa bidhaa kupitia mipaka yote ya nchi ya Tanzania.
“Asas imeanza kulipa kodi tangu mwaka 1951 hivyo tunatambua umuhimu wa kulipa kodi ya serikali, na tunaomba kila mfanyabiashara alipe kutokana na faida itokanayo na biashara yake”, ameeleza Bw. Abri.