Shirika la ndege la taifa la Tanzania, Air Tanzania, limejumuishwa rasmi kwenye Orodha ya Usalama wa Anga ya Umoja wa Ulaya (EU Air Safety List), likiwa miongoni mwa mashirika yaliyopigwa marufuku kufanya safari za anga ndani ya mataifa ya Umoja wa Ulaya.
Uamuzi huu, uliotangazwa tarehe 13 Desemba 2024, umetokana na wasiwasi wa kiusalama uliobainishwa na Mamlaka ya Usalama wa Anga ya Umoja wa Ulaya (EASA).
Kwa mujibu wa taarifa ya Tume ya Ulaya, Air Tanzania haijakidhi viwango vya kimataifa vya usalama wa anga. Hali hiyo imepelekea mamlaka za Ulaya kukataa kutoa idhini ya Uendeshaji wa Shirika la Nchi ya Tatu (TCO).
“Uamuzi wa kuijumuisha Air Tanzania katika Orodha ya Usalama wa Anga ya EU unaonesha dhamira yetu isiyotetereka ya kuhakikisha viwango vya juu vya usalama kwa abiria Ulaya na duniani kote. Tunahimiza Air Tanzania kuchukua hatua za haraka na madhubuti ili kushughulikia masuala haya ya kiusalama. Tumetoa ofa ya msaada kwa mamlaka za Tanzania ili kuboresha usalama wa shirika hili na kufikia viwango vya kimataifa vya usalama wa anga,” amesema Kamishna wa Usafiri Endelevu wa Umoja wa Ulaya, Apostolos Tzitzikostas.
Katika taarifa hiyo, EASA pia ilitangaza mafanikio ya Shirika la Ndege la Kimataifa la Pakistan (PIA), ambalo lilikuwa limepoteza idhini ya TCO mwaka 2020 kutokana na changamoto za usalama. Hata hivyo, baada ya kufanya mageuzi makubwa na kuboresha uwezo wa usimamizi wa usalama wa anga, PIA sasa limeondolewa kwenye vikwazo na linaruhusiwa tena kufanya safari Ulaya.
Kwa sasa, jumla ya mashirika 129 ya ndege yamepigwa marufuku kuruka katika anga za Umoja wa Ulaya (EU). Mashirika 100 ya ndege kutoka nchi 15 yamejumuishwa kwenye orodha hii kutokana na ukosefu wa usimamizi wa kutosha wa usalama kutoka kwa mamlaka za anga za nchi zao.
Mashirika 22 ya ndege ya Urusi yaliongezwa kwenye orodha baada ya anga za EU kufungwa rasmi kwa ndege za Urusi tarehe 27 Februari 2022, kufuatia uvamizi wa Ukraine. Mashirika saba yamejumuishwa kwenye orodha kutokana na wasiwasi mahususi wa kiusalama ambayo ni Air Tanzania (Tanzania), Air Zimbabwe (Zimbabwe), Avior Airlines (Venezuela), Blue Wing Airlines (Suriname), Iran Aseman Airlines (Iran), Fly Baghdad (Iraq) na Iraqi Airways (Iraq).
Mashirika mawili ya ndege, Iran Air (Iran) na Air Koryo (Korea Kaskazini), yanaruhusiwa kufanya safari za anga ndani ya EU, lakini kwa masharti maalum, yakiwa na aina mahususi za ndege zinazokubalika.
Akilizungumzia suala hilo jana Ijumaa Desemba 13, 2024 Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema shirika hilo lipo kwenye majadiliano na mamlaka za Ulaya kwa ajili ya kuyafikia masharti husika.
Ameongeza kuwa tayari wataalamu wa masuala ya anga kutoka EU wamefika nchini na wapo katika mazungumzo ATCL kuona namna ya kupata vibali hivyo.
Tangazo hilo limeibua hisia kali miongoni mwa Watanzania mitandaoni, ambao wameliona kama pigo kwa juhudi za Air Tanzania kupanua safari zake kimataifa, hasa Ulaya. Mwanahabari na mchora katuni maarufu Masoud Kipanya ametoa mtazamo wake, akisema kuwa Afrika inahitaji kujitegemea zaidi na kuwekeza katika uwezo wake wa ndani.
“Ni lazima Afrika ianze kujibeba. Leo unaweza kupanda ndege kutoka Afrika kwenda Ulaya, lakini ni vigumu kupata safari za moja kwa moja kati ya miji ya Afrika. Hili ni somo kwa viongozi wetu,” aliandika Kipanya.
Air Tanzania, maarufu kama “The Wings of Kilimanjaro,” limekuwa likijitahidi kujitanua kama shirika la ndege linaloongoza katika ukanda wa Afrika, likiwa na mipango kabambe ya kupanua huduma zake kimataifa.
Shirika hilo ni mwanachama aliyethibitishwa wa IATA, na linaendesha safari za kimataifa kwenda China, India, UAE, Oman, na Afrika Kusini. Pia linafanya safari kwenda Zambia, Kenya, Visiwa vya Comoro, Zimbabwe, Uganda, Rwanda, Msumbiji, Ethiopia, DRC, Burundi, na lina zaidi ya safari 10 za ndani ya nchi.