Na Joel Maduka, Shinyanga.
Wananchi wa Kata ya Chela Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama mkoani Shinyanga, wamedai wamekuwa wakisumbuka kusafiri na kusafirisha mazao yao kutokana na barabara nyingi za vijiji zilizopo kwenye kata hiyo kuharibiwa na mvua kubwa zilizonyesha msimu wa masika.
Wananchi hao wametoa kilio chao mbele ya Mbunge wa Jimbo la Msalala Iddi Kassim Iddi, ambaye amefika kwenye Kata hiyo na kukutana na wananchi wa kijiji cha Buchembanga, Jomu, Nundu na Mhandu.
Wamesema wamekuwa wakihangaika sana kutokana na sasa barabara nyingi hazipitiki hali ambayo imekuwa ikiwasababisha kusimama kwa kazi za kimaendeleo wanazozifanya pindi mvua zinaponyesha kutokana na miundombinu mingi ya barabara kuharibika.
“Tunakuomba sana fikisha kilio chetu kwa TARURA, TANROAD au hata Serikali kuu au ya Halmashauri, tuna hali mbaya barabara zetu nyingi hazipitiki nyingine kutokana na msimu wa mvua kumalizika zinapitika lakini kwa shida ukiwa na mgonjwa, tunapata shida kubwa kuwafikisha Hospitalini, tunakuomba ulibebe suala la barabara liwe ajenda yako tunajua hujawahi kushindwa, kama tumepata Barabara ndefu ya Kakola hadi Kahama hizi za vijiji tusaidie Mbunge” Alisema Samwel Yegela mkazi wa kata ya Chela.
Aidha wananchi wamesema ubovu wa barabara umekuwa ukisababisha baadhi ya wanawake kujifungulia njiani na hata wagonjwa kushindwa kufika kwenye vituo vya afya na Zahanati kutokana na hali kuwa mbaya zaidi.
Kufuatia kilio cha wananchi, Mbunge wa Jimbo la Msalala Iddi Kassim Iddi amesema tayari serikali ya awamu ya sita kupitia kwa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imetenga fedha ya dharura ya kukarabati barabara zote mbovu na kwamba muda wowote wakandarasi wataanza marekebisho yake.
“Niwaondoe hofu wananchi wangu tunaye Rais msikivu na mwenye upendo wa dhati kwa wananchi wake, nyie ni mashuhuda mmeona mvua zilizonyesha ziliharibu miundo mbinu ya barabara lakini niwaondoe mashaka, fedha nyingi zimetengwa kwa ajili ya kukarabati barabara zote ambazo zimeharibika” Amesema Mbunge Iddi.