Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete, ameupongeza Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake.
Akizungumza wakati wa hafla ya ugawaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu Juni 25, 2025 iliyofanyika katika Chuo cha Marekebisho kwa Watu Wenye Ulemavu cha Sabasaba mkoani Singida. Mhe. Kikwete alisema WCF imekuwa mfano wa taasisi zinazotekeleza kwa vitendo dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kumlinda mfanyakazi na kukuza usawa kwa makundi yote ya jamii
“Nitoe wito Kwa Taasisi nyingine kuiga mfano wa WCF wakurejesha Kwa jamii, iwe ni kwa huduma, vifaa au fursa mbambali” alisema
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, alishukuru Serikali kwa kuwezesha watu wenye ulemavu kupata nafasi zitakazowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii bila kujali hali zao.
Naye Dkt. Mduma amesema Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na kuanzishwa kwa Fao la Utengamao lenye vipengele vitatu ambayo ni utengamao wa kiafya (medical rehabilitation), utengamao wa ujuzi (vocational rehabilitation), na utengamao wa kijamii (social rehabilitation).
Mkuu wa Chuo cha Sabasaba, Fatuma Malenga, amemshukuru Rais Samia kwa kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa vyuo vipya, pamoja na kuwezesha vijana kupitia mikopo ya asilimia 10 kwa ajili ya mitaji.