Latest Posts

LISSU: JESHI KWENYE SIASA NI HATARI KWA DEMOKRASIA AFRIKA

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, amewakosoa vikali wanasiasa na viongozi wa Afrika kwa tabia yao ya kung’ang’ania madaraka kwa maslahi binafsi.

Akizungumza katika kikao cha kujadili masuala ya demokrasia barani Afrika katika Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Makerere, Uganda, Lissu ameainisha mbinu mbalimbali zinazotumiwa na viongozi wa Afrika kuendeleza udhibiti wa kisiasa kwa kisingizio cha kulinda katiba.

Kulingana na kituo cha habari cha DW, Lissu ameeleza kuwa viongozi wengi wa Afrika wanaanza kwa kuhamasisha uzalendo na kuungwa mkono na wananchi, lakini wanapopata madaraka, hujenga mifumo inayodhoofisha demokrasia. Amesema mfano halisi ni serikali ya Uganda ambayo imehusisha jeshi katika siasa za nchi, hali inayohatarisha misingi ya utawala wa kidemokrasia.

Katika hotuba yake, Lissu amesema kuwa Mwalimu Julius Nyerere alitoa mchango mkubwa katika uongozi wa Afrika, lakini baadhi ya viongozi waliiga mifumo yake ya udhibiti wa taasisi za kisiasa, kijamii, na kiuchumi kwa manufaa yao binafsi.

“Kuhusika kwa majeshi katika siasa za taifa ni hatari sana, na Mwalimu Nyerere aliwafunza viongozi wengi wa Afrika namna ya kutumia majeshi katika kudhibiti upinzani. Itakuwa vigumu kuondoa hali hiyo,” amesema Lissu.

Ameeleza kuwa Rais wa Uganda Yoweri Museveni alilelewa kisiasa na Nyerere, na kwamba mifumo ya kisiasa anayoitumia sasa aliiga kutoka kwake.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa na wasomi na wanafunzi wa sheria, mjadala umeibuka kuhusu uhuru wa kujieleza kama msingi wa demokrasia.

Baadhi ya wasomi wameeleza kuwa changamoto kubwa ya utawala wa Afrika ni pale wananchi wanaponyimwa uhuru wa kujieleza na kushiriki maamuzi ya taifa.

Hata hivyo, mmoja wa wasomi hao, Dk. Daniel Ruhweza, amesema kuwa japo Nyerere aliwahi kufanya maamuzi pasipo kuwashirikisha wananchi, baadaye wengi walikuja kuona faida yake.

“Wakati mwingine kiongozi anafahamu kile ambacho raia hawawezi kukubaliana nacho, lakini baadaye kinakuwa na manufaa kwa taifa,” amesema Dk. Ruhweza.

Lissu amewataka viongozi wa Afrika kuiga mfano wa Nyerere wa kuheshimu ukomo wa madaraka na kuachia nafasi baada ya kuhudumu kwa mihula miwili, badala ya kung’ang’ania madaraka.

“Angalau wajifunze yale mazuri ya Nyerere, hasa ya kuachia madaraka kwa hiari na kuheshimu utawala wa awamu mbili,” amesema Lissu.

Pia amesisitiza kuwa wanasiasa na wanasheria wanapaswa kushirikiana katika kuhakikisha kunakuwepo na utawala wa kidemokrasia, haki za binadamu, na kulinda katiba za nchi zao.

Latest Posts

Don't Miss

Stay in touch

To be updated with all the latest news, offers and special announcements.

error: Content is protected !!