Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, ametoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya ulaghai, wizi na utapeli ndani ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), akisisitiza kuwa hatasita kuchukiwa na yeyote katika kulinda uaminifu wa mfumo huo.
Akizungumza na wahariri na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Februari 2, 2026, Mchengerwa amesema ulaghai katika bima ya afya si wizi wa fedha pekee, bali ni “wizi wa huduma na maisha” ya Watanzania.
Waziri amebainisha kuwa mfumo wa Bima ya Afya kwa Wote unakabiliwa na maadui wawili: maradhi na ulaghai. Amesema huku serikali ikipambana na maradhi kwa kutoa tiba na kinga, vita dhidi ya ulaghai inahitaji ushirikiano mkubwa na waandishi wa habari za kiuchunguzi ili kubaini ubadhirifu unaofanyika kwenye vituo vya kutolea huduma na kwenye madai ya malipo.

“Uandishi wa habari za kiuchunguzi katika sekta ya afya itakuwa ni kinga ya mfumo bila kinga mfumo huumwa. Sitakubali chini ya uongozi wangu NHIF ichezewe sitakubali hata kidogo, na hili nalisema, nimelisema mara nyingi na nitaendelea kusisitiza…Kwenye hili nipo tayari kuchukiwa na kila mmoja, niko tayari wala sina tatizo”, amesisitiza Waziri Mchengerwa.
Waziri amewapa waandishi wa habari hadhi ya “macho ya wananchi,” akiwataka kufanya kazi kama doria katika sekta ya afya. Amefafanua kuwa ubadhirifu mara nyingi huanzia kwenye uhalisi kama kwenye risiti, foleni za wagonjwa, na malalamiko ya wananchi, maeneo ambayo uandishi wa kiuchunguzi unaweza kuona na kuzuia mapema kabla ya madhara makubwa kutokea.
Ameeleza kuwa uaminifu wa NHIF ndio uimara wa taifa, kwani bila uaminifu huo, hata sera bora za kisheria zitashindwa kutekelezeka kijamii. Mchengerwa amewahakikishia waandishi kuwa milango yake iko wazi kwa ajili ya ushirikiano ili kuhakikisha huduma za afya zinaboreshwa na kila senti ya mwananchi inatumika kwa makusudi yaliyokusudiwa.